Thursday, November 22, 2012

Mhe.MEMBE ANENA KUHUSU M23

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe:Tanzania inalaani kitendo cha kikundi cha M23 kuteka mji wa Goma na kutishia kuteka miji mingine ya Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya(DRC) Kongo wakati mazungumzo yakiwa bado yanaendelea na tunawataka Waasi kuondoka mara moja.-{VIDEO}


Mhe. Bernard K. Membe (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, akitoa msimamo wa Tanzania kuhusu vitendo vya kikundi cha waasi cha M23 kilichopo Mashariki mwa Congo DRC. Kushoto ni Balozi Simba Yahya.
Mhe. Bernard K. Membe (Mb) (katikati) akilaani mashambulizi ya kikundi cha waasi cha M23 kilichoteka mji wa Goma, Mashariki mwa Congo DRC. Waziri Membe aliyasema hayo alipokuwa katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika leo katika Ukumbi wa Mikutano, Wizara ya Mambo ya Nje, mjini Dar es Salaam. Kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. John M. Haule na Kushoto ni Balozi Simba Yahya, Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati, Wizarani.Picha na Tagie Daisy Mwakawago-Wizara ya Mambo ya Nje

--
Na ALLY KONDO SEIF
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb) amelaani kitendo cha kikundi cha M23 kuteka mji wa Goma na kutishia kuteka miji mingine ya Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Mhe. Waziri alitoa msimamo huo wakati alipozungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam tarehe 22 Novemba, 2012.

Mhe. Waziri alisema kuwa hali ya usalama mjini Goma ni mbaya kutokana na mashambulizi hayo ya M23 na hali hiyo ikiachwa iendelee, Tanzania itaathirika kwa kiasi kikubwa kwani watu wengi watakimbilia hapa nchini kama wakimbizi.

Aidha, Mhe. Waziri alisikitishwa na kikundi cha M23 cha kupuuza wito uliotolewa na viongozi wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Sekretarieti ya Nchi za Maziwa Makuu (ICGLR) wa kusitisha mapigano hayo.

Mhe. Waziri aliendelea kueleza kuwa Tanzania inasikitishwa na jeshi la Umoja wa Mataifa la MONUSCO lililopewa jukumu la kulinda amani Mashariki ya DRC kwa kushindwa kuchukuwa hatua za kukomesha mashambulizi hayo na badala yake kuwa mashuhuda wa mashambulizi yanayofanywa na kikundi cha M23 dhidi ya Serikali na wananchi wa kawaida.

Aliuomba Umoja wa Mataifa utoe mamlaka ili MONUSCO iwe na uwezo wa kisheria wa kukabiliana na waasi wa M23 kama sura ya 7 ya Umoja wa Mataifa inavyoelekeza badala ya kutumia sura ya 6 ya Umoja wa Mataifa inayosisitiza umuhimu wa kulinda amani bila kujibu mashambulizi.

Kuhusu jitihada zinazofanywa na SADC kwa kushirikiana na ICGLR za kutafuta suluhu ya kudumu ya mgogoro huo, Mhe. Membe alisema kuwa mwezi Agosti, 2012 Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hizo walikutana mjini Kampala, Uganda na kuamua kuunda kikosi cha kulinda amani ili kitumwe Mashariki ya DRC. Tanzania iliahidi kuchangia batalioni moja lakini kikosi hicho cha kulinda amani hakijapata ridhaa ya Umoja wa Mataifa.

Umoja wa Mataifa hautaki kutoa ridhaa ili kikosi hicho kipelekwe DRC kwa hoja kuwa tayari jeshi la Umoja wa Mataifa lipo nchini DRC.

Mhe. Waziri alihitimisha Mkutano wake kwa kutoa taarifa kuwa nchi za SADC na ICGLR zitakuwa na mkutano nchini Uganda kuanzia siku ya Ijumaa tarehe 23 Novemba, 2012 kujadili hatua za haraka za kuchukuwa ili kukabiliana na mzozo wa DRC.

No comments:

Post a Comment